Dunga amsikitikia Maximo
Na Dominic Isiji
KOCHA mkuu wa timu ya soka ya Brazil, Carlos Dunga, ameeleza kusikitishwa kwake na kuondoka kwa kocha mkuu wa timu ya Tanzania, Taifa Stars, Marcio Maximo ambaye mkataba wake unakamilika mwezi ujao.
Tayari Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limemtangaza Jan Poulsen raia wa Denmark kama mrithi wa Maximo na ataingia mkataba wa miaka miwili Agosti Mosi mwaka huu.
Akizungumza jijini Dar es Salaam juzi baada ya mechi ya kihistoria kati ya Taifa Stars na mabingwa wa dunia mara tano, Dunga alisema Maximo amefanya kazi kubwa kuibadilisha Taifa Stars.
“Ninampongeza Maximo kwa kazi nzuri aliyofanya kwa timu hii (Taifa Stars) ila cha kusikitisha ni kwamba anamaliza muda wake,” alisema nahodha huyo wa zamani wa Brazil.
Dunga alikiri kufurahishwa na mchezo wa juzi ambao Brazil ilishinda 5-1 akisema kuwa alihitaji kucheza na timu yenye kasi.
Alisema kuwa Maximo ameweza kutengeneza timu nzuri yenye kucheza na mipango na kwa kasi jambo ambalo liliwapa taabu mabeki wake na wakati mwingine kufanya washindwe kupanda wakihofia kuzidiwa kasi kwa mashambulizi ya kushitukiza.
Katika mchezo wa juzi, Brazil ilitumia kikosi chake cha kwanza ambacho kilimkosa mchezaji mmoja tu, kipa Julio Cesar anayeuguza jeraha ya mgongo na alishindwa kusafiri na timu hiyo kuja Dar es Salaam.
Dunga alisema kuwa nia ya Brazil kucheza na Zimbabwe na Tanzania kama maandalizi yao kuelekea Kombe la Dunia linaloanza kesho kutwa nchini Afrika Kusini, ilikuwa ni kujipima nguvu na kasi ya timu pinzani hususan za Afrika.
“Nchi za Afrika zinasifika kuwa na wachezaji wenye nguvu na kasi na nimeridhika na michezo yetu miwili ya kimataifa ya kirafiki kwa sababu Zimbabwe walicheza mpira wa nguvu na Tanzania mpira wa kasi vitu ambavyo wachezaji wangu waliweza kuvimudu,” alisema.
Hadi mechi ya juzi, Brazil mara ya mwisho kwa nyavu zao kutikiswa ilikuwa Oktoba mwaka jana ambapo walishinda 2-1 katika mchezo wao wa kufuzu kuelekea Kombe la Dunia.
Maximo
KOCHA mkuu wa timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars, anayemaliza muda wake Marcio Maximo amesema kuwa mrithi wake atapata kazi rahisi.
Nafasi ya Maximo itachukuliwa na Jan Poulsen raia wa Denmark ambaye anatarajiwa kuingia mkataba wa miaka miwili Agosti 1 mwaka huu.
Akizungumza baada ya mechi ya juzi kati ya Taifa Stars na Brazil uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kushuhudiwa na Rais Jakaya Kikwete, Maximo alisema mrithi wake hatakuwa na shida ya kuanza kuunda kikosi.
Alisema kuwa anaondoka huku akimwachia Poulsen kikosi imara cha Taifa Stars na timu nzuri za vijana.
“Sidhani kama (mrithi wangu) atapata shida na ninategemea kuwa atayaendeleza mazuri niliyoanzisha ila kama atataka kuanza upya, hiyo itakuwa jukumu lake,” alisema Maximo huku akimtakia kila la heri Poulsen .
Akizungumzia kuhusu mechi ya juzi, Maximo alisema amefurahishwa na wachezaji wake licha ya kwamba walilazimika kucheza michezo miwili muhimu ndani ya saa 24.
Stars walifunga na Rwanda 1-0 Jumapili jijini Kigali na kuyaaga michuano ya Kombe la Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN) kwa jumla ya mabao 2-1 na siku iliyofwata wakafungwa 5-1 na mabingwa wa dunia mara tano Brazil katika mechi ya kihistoria.
Maximo alisema ijapokuwa anaondoka, matarajio yake ni kwamba Taifa Stars itacheza mechi nyingi za kirafiki kama ile ya Brazil ili kuwakomoza wachezaji.
Alisema kuwa mechi dhidi ya Brazil ilikuwa darasa tosha ya ni nini kinachotakiwa kwa wachezaji ili nao pia waweze kucheza soka la kulipwa.
More Latest News
-
Daladala latumbukia mtoni Dar ABIRIA 21 waliokuwa wakisafiri kutoka Buguruni kwenda Mbagala jijini...
-
Umeyasikia ya Tatu Ntimizi? BAADHI ya wananchi wa Jimbo la Igalula ambao ni wanachama wa Chama...
-
Hispania yaweka historia HISPANIA imekuwa taifa la nane kushinda Kombe la Dunia baada...
- 1
- 2
- 3
- 4
Advertisement

cartoons


